Friday 2 March 2012

Ishara Na Miujiza Ya Mwenyezi Mungu


Katika maisha ya wanaadamu wote, kutoka wakati wa ujana na utoto hadi wakati wanapofariki, ishara za Mwenyezi Mungu mmoja peke Yake wa kweli zinaonyeshwa kwao katika maeneo yote ya ardhi, hata katika nafsi zao mpaka ibainike kwao kuwa yupo Mwenyezi Mungu mmoja tu wa kweli Allah (Subhaanahu wa Ta'ala). Mwenyezi Mungu Anasema katika Qur’ani:

Tutawaonyesha Ishara Zetu katika upeo wa mbali na katika nafsi zao wenyewe mpaka iwabainikie kwamba haya ni kweli. Je! Haikutoshi kwamba Mola wako Mlezi kuwa Yeye ni Shahidi wa kila kitu? 
Q 41: 53
Hapa tunatoa mfano jinsi Mwenyezi Mungu Anavyompatia ishara mtu mmoja kwa upotevu kwa kuabudu masanamu. Katika eneo la kusini mashariki mwa msitu wa Amazon huko Brazil, Amerika Kusini, kabila la asili lisiostaarabika lilijenga kibanda kipya ili kumpatia makazi sanamu-mtu, Skwatch, likiwakilisha mungu mkubwa kabisa wa uumbaji wote.
Siku ya pili kijana mmoja aliingia katika kibanda hicho ili kutoa heshima zake kwa mungu. Alipokuwa katika hali ya kusujudu kwa jinsi alivyofundishwa kuwa hilo sanamu ni muumba na mlezi wake, na mwenye kuruzuku, mara aliingia mbwa mzee, hafifu na mwenye upele na aliyejawa na viroboto kwenye kibanda hicho. Kijana huyo alinyanyua uso wake kwa wakati muafaka, wakati tu wakumuona mbwa huyo akinyanyua mguu wake wa nyuma na kulikojolea sanamu hilo.
Kijana alimfukuza mbwa huyo katika hekalu kwa ghadhabu kubwa mno; lakini hasira na ghadhabu ilipofifia alitambua kuwa sanamu hawezi kuwa mola wake mlezi wa ulimwengu mzima. Mwenyezi Mungu ni lazima awe kila pahala, alihitimisha. Ajabu kama inavyoonekana, mbwa kulikojolea sanamu ilikuwa ni ishara kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa kijana huyo. Ishara hii ilikuwa na risala ya Mwenyezi Mungu kuwa anachokiabudu ni cha uwongo. Tukio hili lilimuacha huru kijana huyo na utumwa wa kufuata ada alizofundishwa za kuabudu mungu wa uwongo. Matokeo yake ni kuwa huyu kijana alichaguzishwa: ama kutafuta mungu wa kweli au kuendelea katika upotevu wa njia zake.
Allah (Subhaanahu wa Ta'ala) Anatutajia kiu aliyokuwa nayo Nabii Ibraahim (‘Alayhis Salaam) katika juhudi ya kumtafuta Mwenyezi Mungu kama mfano wa wale wenye kufuata ishara Zake jinsi wanavyoongoka (na hivyo kufuata njia nyoofu na ya sawa). Allah (Subhaanahu wa Ta'ala) Anasema:
 “Na kadhaalika Tulimwonyesha Ibraahim ufalme wa mbingu na ardhi, na ili awe miongoni mwa wenye yakini. Na ulipomuingilia usiku akiona nyota, akasema: Huyu ni Mola Mlezi wangu. Ilipotua akasema: Siwapendi wanaotua. Alipouona mwezi unachomoza alisema: Huyu ndiye Mola Mlezi wangu. Ulipotua akasema: Kama Mola Mlezi wangu hakuniongoa, nitakuwa katika kaumu waliopotea. Na alipoliona jua linachomoza akasema: Huyu ndiye Mola Mlezi wangu. Huyu mkubwa kuliko wote. Lilipotua, alisema: Enyi watu wangu! Mimi simo katika hayo mnayofanyia ushirikina. Hakika mimi nimeuelekeza uso wangu sawa sawa kwa aliyeziumba mbingu na ardhi, wala mimi si miongoni mwa washirikina Q 6: 75 – 79
Kama ilivyotajwa hapo awali, Manabii walitumwa kwa kila taifa na kabila kuunga mkono itikadi ya kimaumbile ya mwanadamu kwa Mwenyezi Mungu na mwelekeo wa silica aliozaliwa nao mwanadamu wa kumuabudu Yeye, vile vile kutilia nguvu ukweli wa kutoka kwa mungu. 
Kwa ishara za kila siku zilizodhihirishwa na Mwenyezi Mungu. Japokuwa mafunzo mengi ya Manabii hawa yaligeuzwa, sehemu zinazoonyesha vifungu zilizoteremshwa na Mwenyezi Mungu zimebaki bila ya waa na zimewatumikia wanaadamu kuwaongoza katika kuchagua baina ya ukweli na uwongo, na haki na batili. Ushawishi wa risala zilizofunuliwa na Mwenyezi Mungu kupitia kwa zama zote zinaweza kuonekana katika “Amri Kumi” za Uyahudi katika Taurati ambazo baadaye zilichukuliwa na kuingizwa katika mafunzo ya Ukristo. Vile vile kuwepo kwa kanuni dhidi ya mauaji, wizi na uzinzi katika jamii nyingi sana kote duniani, katika zama za kale na sasa.
Matokeo kwa ishara za Mwenyezi Mungu kwa wanaadamu kupitia kwa zama zote zikichang’anywa na wahyi Wake kupitia kwa Manabii Wake, wanaadamu wote wamepatiwa fursa ya kumtambua Mwenyezi Mungu mmoja tu wa kweli.
Kwa hiyo, kila nafsi itahesabiwa kwa itikadi yake kwa Mwenyezi Mungu na kukubali kwake kwa Dini ya kweli ya Mwenyezi Mungu, Uislamu, ambayo ina maana ya kunyenyekea na kutii amri za Allah (Subhaanahu wa Ta'ala).

No comments:

Post a Comment

Qur'an 5:32